Mnenguaji  wa Kundi la Kanga Moko, Zawia Hamis


DIANA Semhando na Zawia ambao ni mastaa wa kundi maarufu la minenguo Khanga Moja (ambao majuzi walipata msukosuko wa kufyatuliwa risasi mtaani), wamepata lebo na studio ya Fire Music ya jijini Dar es Salaam na kupakua wimbo unaokwenda kwa jina la “Ayaya” ambao utawatambulisha katika ulimwengu mwingine wa sanaa – ulimwengu wa uimbaji.

Mkurugenzi mtendaji wa Fire Music, Masoud Kandoro, ameiambia Saluti5 kuwa wimbo huo upo katika hatua za mwisho na kwamba wakali hao ambao watajitambulisha kama WADADA WAWILI wameutendea haki wimbo huo.

“Ni wimbo mkali, Wadada Wawili wameimba vizuri na kilichobakia ni mambo madogo madogo, tunataraji kupata rap fupi fupi za Msafiri Diuof ili kuunogesha zaidi,” alisema Kandoro.

Wimbo huo umetungwa na kupangiliwa sauti na H- Mbizo ambako ndani yake utakutana na mistari kama “Penye miti hakutaki wajenzi, panataka wakwezi”, “Dukani kumejaa vipodozi kuzaa kunataka malezi”, “Taarab haionogi mapozi inanoga mashauzi”.

H- Mbizo ndiye aliyetunga wimbo wa “Majanga” uliompatika sifa kibao mwanadada Snura.
Mnenguaji  wa Kundi la Kanga Moko, Zawia Hamis
 
Top